Thursday, May 17, 2018

LULU AUVAA MOTO WA MAMA KANUMBA


Wakati chozi la furaha ya kupunguziwa adhabu likiwa bado halijamkauka muigizaji Elizabeth Michael ‘Lulu’, mama wa aliyekuwa mchumba wa muigizaji huyo, marehemu Steven Kanumba, Flora Mtegoa amefungua kinywa chake na kuliamsha dude kuhusu tukio hatua hiyo.

Lulu aliyekuwa akitumikia kifungo chake cha miaka miwili katika Gereza la Segerea, alipunguziwa adhabu hiyo Mei 12, mwaka huu kufuatia amri ya Mahakama Kuu huku taarifa ya magereza ikieleza kuwa mrembo huyo, alipunguziwa robo ya kifungo chake kutoka kwenye msamaha wa Rais Dk John Pombe Magufuli.

Msamaha huo aliutoa Rais, Aprili 26, mwaka huu mjini Dodoma katika Sherehe za Maadhimisho ya Miaka 54 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambapo alitoa msamaha huo kwa wafungwa mbalimbali nchini akiwemo Lulu aliyefungwa kwa kosa la kumuua bila kukusudia, Kanumba.


LULU AFICHWA
Mara baada ya mrembo huyo kutoka gerezani Jumamosi, Risasi Mchanganyiko lilifanya jitihada za makusudi kumtafuta mrembo huyo pamoja na familia yake lakini ilibainika kuwa ni ngumu huku ikionekana walidhamiria kutomuanika hadharani mpaka hapo watakapoona inafaa.

Jumapili iliyopita, Risasi Mchanganyiko lilijaribu kuwatafuta watu wa karibu na Lulu akiwemo mama yake mzazi, Lucrecia Karugila ambaye alitoa maneno ya shombo huku akiomba aachwe kwani yeye hana taarifa za Lulu kutoka gerezani na hapendi mambo aliyoyaita kuwa ni ya kidaku.

Risasi Mchanganyiko: Naongea na mama Lulu?

Mama Lulu: Hapana mimi ni Farida wa Tanga. Utakuwa umekosea namba.

Baada ya muda mfupi…
Risasi Mchanganyiko lilifanya uchunguzi wa sekunde kadhaa na kugundua namba ile ambayo ilijibu kuwa ni Farida wa Tanga ni ya mama Lulu baada ya kuingia kwenye upande wa WhatsApp na kugundua ni mama Lulu kisha kumpigia kwa mtandao huo.

Risasi Mchanganyiko: Mama yangu hakuna sababu ya kutuzungusha, tafadhali tueleze tu ukweli, Lulu ametoka?

Mama Lulu: Ametoka wapi? Hebu acha mambo yako ya udaku. Ametoka wewe upo naye? Mimi kama mama yake mzazi sina hiyo taarifa, wewe umezitoa wapi? Acheni mambo yenu bwana, tena nakuambia sitaki uandike hizo habari. Nitakuja hapo ofisini kwenu, nitamueleza bosi wenu.

Risasi Mchanganyiko likaachana na mama Lulu na kumgeukia rafiki mkubwa wa familia, muigizaji Mahsein Awadhi ‘Dk Cheni’ ambaye naye alikanusha taarifa za Lulu kutoka gerezani.

“Nyinyi ni watu wangu. Angetoka ningewaambia,” alisema Dk Cheni.

Baada ya familia hiyo kuonekana ‘kumficha’ Lulu, Jumatato Jeshi la Magereza lilithibitisha Lulu kupunguziwa adhabu ambapo Risasi Mchanganyiko lilimgeukia mama mama Kanumba ambaye aliporomosha moto wa aina yake kupitia simu ya mkononi.


HUYU HAPA MAMA KANUMBA
“Nawashukuru wote waliofanikisha kutoka kwa Lulu lakini wakae wakitambua kwamba sijafurahia kabisa, imeniuma maana naona kama haki haijakaa sawa.

“Najua Lulu na ndugu zake wanasherehekea sasa hivi lakini wakae wakijua sijafurahishwa na kilichotokea. Kanumba alikuwa akiwalipia kodi Lulu na mama yake lakini leo wanafanya haya wanayoyafanya kweli? Bora hata wangemuacha atumikie kidogo adhabu lakini namuachia Mungu,” alisema mama Kanumba huku sauti yake ikiashiria kuwa analia.

VITA UPYA
Hii si mara ya kwanza mama Kanumba kumcharukia Lulu, kabla ya mrembo huyo kuhukumiwa, bi mkubwa huyo amekuwa akimlalamikia kwa kitendo chake cha kutomjali huku akijua fika yeye ni mama ambaye angeweza kuwa mkwewe kama kifo cha mwanaye kisingetokea.Kutokana na kauli hiyo, ni dhahiri sasa bifu la mama Kanumba na familia ya Lulu litakuwa limekolea upya!

TUJIKUMBUSHE
Lulu alihukumiwa kwenda jela miaka miwili Novemba 13, 2017 baada ya kukutwa na hatia ya kumuua bila kukusudia, aliyekuwa mpenzi wake, Kanumba kosa ambalo alidaiwa kulifanya Aprili 7, 2012 nyumbani kwa marehemu, Sinza-Vatican jijini Dar es Salaam.

No comments: