Friday, March 9, 2018

RAIS KENYATTA, ODINGA WAKUTANA LEO, WAAPA KUFANYA KAZI PAMOJA

Rais Uhuru Kenyatta (kushoto) akiteta jambo na Raila Odinga.

Kwa mara ya kwanza baada ya Uchaguzi Mkuu nchini Kenya uliofanyika Oktoba 2017 na kuleta mkanganyiko mkubwa wa kisiasa nchini humo, Rais Uhuru Kenyatta na Kiongozi wa Upinzani wa NASA Raila Odinga leo Machi 9, 2018 wamekutana rasmi na kuzungumza.

Viongozi hao wamekutana na kuzungumza kuhusu kuacha tofauti zao za kisiasa na kutanguliza maslahi ya wananchi wa nchi hiyo kwanza kwa kufanya kazi pamoja kurudisha amani.

“Maisha yetu ya baadaye hayawezi kupimwa kwa Uchaguzi Mkuu unaofuata bali utulifu wa nchi yetu na hali nzuri ya watu wetu, demokrasia ni mchakato ambao, hiari ya watu inasikilizwa lakini maslahi ya taifa lazima yatawale.” – Uhuru Kenyatta

Kwa upande wake Raila Odinga ameeleza kuwa “tukiendelea kuwa wabinafsi na waharibifu, hakuna kiwango chochote cha mageuzi ya kitaasisi ambacho kitaboresha maisha yetu.”

Inaelezwa kuwa wawili hao wamekubaliana kushirikiana katika agenda 9 mahususi, na ipo Kamati iliyoundwa itakayohusisha wajumbe wa pande zote mbili ili kuanzisha programu ya kuwaunganisha tena wananchi ambao walitengwa na milengo ya kisiasa katika kipindi cha uchaguzi.

No comments: